KITENDO cha timu ya Simba kutotumia magari yao kwenye safari zake za hapa na pale pamoja na kwenda nayo uwanjani kwenye mechi kimeanza kuwashangaza wengi huku wakiwa gumzo kwenye mitandao ya kijamii.
Mabasi ya klabu ya Simba hayajashikiliwa kama inavyoenezwa kwenye mitandao ya kijamii bali yapo katika ukarabati
Meneja wa Habari na Mawasiliano klabu ya Simba, Ahmed Ally alisema mabasi yao hayaonekani kwa sababu yako gereji na sio kama ambavyo watu wamekuwa wakizungumza kuhusu kushikiliwa kwa sababu za kukiuka mikataba
Ahmed amesema taarifa zaidi zinaweza kutolewa na viongozi wa juu wa klabu lakini taarifa rasmi aliyonayo ni kuwa mabasi hayo yako gereji
"Wenye mamlaka ya kuzungumzia hayo ni viongozi wa Simba na mimi niseme tu wazi kwa mashabiki wetu kwamba mabasi yapo gereji pale Vingunguti, na yatakapokamilika kufanyiwa ukarabati mtayaona," alisema Ahmed
Katika siku za karibuni Simba imeonekana kutumia usafiri wa mabasi madogo 'coaster' kupeleka wachezaji uwanjani kwenye mechi na hata mazoezini kule Mo Simba Arena, Bunju